Balozi Seif kuwa mgeni rasmi maonesho ya wakulima (nane nane) Dole Magharibi A Unguja

MAKAMU Wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idi anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa sherehe za maonyesho ya wakulima ( nane nane ) yatakayofanyika Dole wilaya ya magharibi A .
Hayo aliyasema Waziri wa Kilimo Maliasili Mifugo na Uvuvi Rashid Ali Juma katika viwanja vya maonyesho ya sikukuu ya wakulima Dole wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mipango ya maonyesho hayo.
Alisema sherehe hizo maalum ya kuadhimisha siku ya wakulima duniani zitawafanya kukutana wakulima na kuona uzoefu, ufundi na ustadi katika kutumia njia za kisasa na kuondoa njia za kawaida ambazo walikuwa wamezoea.
“Hivi sasa ukulima umekuwa wa kisasa kwa kutumia sehemu ndogo ya ardhi kupanda mpunga na baada ya muda mfupi kuvuna mpunga mwingi”. Alisema Waziri huyo.
Aidha alisema kilimo Zanzibar ni uti wa mgongo huchangia katika sekta hiyo kukuza pato la kiuchumi na pia kukuza utalii kwa kupata vyakula kwani mazao mengi huwa kivutio kwao.
Pia alisema asilimia 80 ya wazanzibar wameweka ajira zao kwenye sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi hivyo aliwataka wananchi wajishirikishe kwenye kilimo kwa kuweza kujiongezea pato lao la maisha.
Alisema miundo mbinu imeboreshwa , maji safi salama na huduma za usalama zitazidi kuhakikisha usalama wa raia na mali zao na pia vyakula mbali mbali vitapatikana .
Aliwaomba wakulima na wafanya biashara wafugaji kushiriki kwa wingi katika maonyesho hayo ambapo yatayoweza kuwapatia ujuzi wa kila aina na kuweza kupata viwanda na pia kukuza uchumi .
Vile vile alisema Serikali ya Mapinduzi imeiwekea sekta ya kilimo kipaumbele kwa lengo kukuza kilimo na pia kuona wananchi wake wanaweza kufaidika na huduma hizo za kilimo uvuvi na ufugaji.
Zaidi ya milioni mia moja na hamsini zimetengwa kwa kukamilisha maonyesho ya sherehe ya maonyesho ya wakulima ambapo kauli mbiu ya mwaka huu WEKEZA KATIKA KILIMO UVUVI NA UFUGAJI KWA MAENDELEO YA VIWANDA.
Maonyesho hayo hufanyika kila mwaka duniani kote ifikapo tarehe 8-8 kila mwaka.
No comments